Advert


java

Connectify - Turn Your PC into a Wi-Fi Hotspot. Install now!

Thursday, June 26, 2014

MBUNGE WA KIGAMBONI DR. F. ANDUNGULILE AONGEA NA TANESCO KUHUSU KERO ZA UMEME

Mrejesho wa suala la umeme kwa maeneo mbalimbali ya Jimbo la Kigamboni

Siku ya Jumatatu tarehe 23.06.2014 nilifanya mkutano na uongozi wa Tanesco ngazi ya Mkoa wa Temeke na Wilaya ya Kigamboni. Mambo yaliyojadiliwa ni pamoja na:

Kukatika kwa mara kwa mara kwa umeme Umeme mdogo kwa baadhi ya maeneo Uunganishaji wa umeme kwa wateja wapyaMiradi mipya ya umeme kwa Jimbo la Kigamboni

1. KUKATIKA KWA MARA KWA UMEME JIMBO LA KIGAMBONI

Umeme unaopatikana kwa wateja wa Jimbo la Kigamboni unatoka sub-station ya Ilala. Umeme huu pia husambazwa kwa maeneo ya Temeke, Mbagala na Mkuranga. Kutokana na ongezeko kubwa la mahitaji pamoja na uchakavu wa miundombinu, kumekuwa na ukatikaji wa umeme mara kwa mara.

Tanesco walinieleza kuwa hatua ambazo wanachukua kuondoa tatizo hili ni pamoja na maboresho ya miundombinu, kusafisha njia unaopita umeme huo kwa kukata miti na matawi na kujenga sub-station mpya maeneo ya Mbagala. Kukamilika kwa sub-station ya Mbagala utapunguza utegemezi uliopo sasa kwa sub-station ya Ilala. Kazi ya ujenzi wa sub-station mpya unatarajia kukamilika mwezi Disemba mwaka huu.

2. UMEME MDOGO KWA BAADHI YA MAENEO (LOW VOLTAGE)

Kuna baadhi ya maeneo kama vile Kijichi na Magogoni kumekuwa na tatizo la umeme mdogo. Tanesco walinitaarifu kuwa kuna mpango wa kufanya “voltage improvement” kwa kufanya “phase addition” na kuongeza transfoma nyingine mbili maeneo ya Magogoni. Transfoma zipo na ninatarajia kazi hii itaanza hivi karibuni. Kwa upande wa Kijichi, pamoja na “voltage improvement” bado kutakuwa na tatizo. Suluhu ya kudumu itakuwa kukamilika kwa sub-station ya Mbagala.

Tulikubaliana kuwa kazi hii iwe imekamilika ndani ya miezi mitatu ijayo.

3. UMEME KWA WATEJA WAPYA

Nimekuwa nikipokea malalamiko mengi toka kwa wananchi wengi ambao wamekuwa wakisubiri muda mrefu kupata huduma ya umeme. Malalamiko yamekuwa yakitoka Kibada, Gezaulole, Toangoma, Saku, Rufu na Kiponza.

Uongozi wa Tanesco ulinihakikishia kuwa maandalizi yamekamilika kwa ajili ya usambazaji wa umeme kwenye maeneo ya Kibada (blocks 14,15,16,17,18,19,20).  Waliahidi kukamilisha kazi hii ifikapo mwezi Septemba 2014.

Niliwataka ndani ya wiki tatu (3) kunipa mikakati yao ya kuwapatia umeme wananchi walioomba toka maeneo ya Gezaulole, Mbwamaji, Kizani, Mwera, Kibada(blocks zilizobaki), Ponde, Goroka Kalakala, Masaki na  Malela. Uongozi wa Tanesco uliahidi kufanya hivyo kwani miradi hii imeshatengewa Bajeti zake. Pia, Tanesco haina uhaba wa vifaa vya kuunganisha umeme kwa sasa.

4. MIRADI MIPYA YA UMEME JIMBO LA KIGAMBONI 

Uongozi wa Tanesco ulinitaarifu kuwa maombi yangu ya kutaka Kata za Kimbiji na Pemba Mnazi kuingizwa kwenye mradi wa Umeme Vijijini (REA) yamekubaliwa na sasa kata hizi zitaanza kupata huduma ya umeme.

Kama nilivyoeleza hapo juu, umeme wa sasa kwa Jimbo la Kigamboni hutoka Ilala, ujenzi wa Sub-Station ya Mbagala unaendelea na unatarajia kukamilika mwezi Disemba, 2014. Kukamilika kwa kituo kutafanya baadhi ya maeneo ya Jimbo la Kigamboni kujitegemea kwa huduma ya umeme na pia kuondokana kukatika katika mara kwa mara kwa umeme kama ilivyo sasa.

Vile vile Tanesco ipo kwenye mchakato wa kutafuta eneo katika Tarafa ya Kigamboni kwa ajili ya ujenzi wa sub-station mpya. Katika mwaka huu wa fedha hakuna fedha iliyotengwa kwa mradi huu. Lengo ni kuingiza ujenzi wa sub-station kwenye bajeti ijayo.

Aidha, niliwataka uongozi wa Tanesco kufanya maandalizi ya awali kujua gharama za kufikisha umeme katika maeneo ya Mwasonga, kata ya Kisarawe II ili makisio haya yaingizwe bajeti ya mwakani.Tulikubaliana zoezi hili kufanyika ndani ya miezi mitatu.

5. HITIMISHO 

Shirika la Tanesco halina uhaba wa vifaa kwa sasa. Niliwataka Tanesco Kigamboni kuandaa mpango kazi wa usambazaji wa huduma ya umeme kwa wateja wapya  ambayo itanisaidia kufuatilia utendaji kazi wao; kuboresha mawasiliano na mahusiano na wateja pindi umeme unapokatika au pale wateja wanapofika kuuliza kuhusu hatma ya maombi yao. Kwa vile, Tanesco ina uhaba wa vikosi vya kuunganisha umeme kwa wananchi, niliwashauri waangalie uwezekano wa kutumia wakandarasi binafsi (outsourcing) baadhi ya kazi hizi.

Kwa wananchi wa Kibada, Toangoma na Gezaulole kwa maeneo mliyoniletea orodha zenu, ndani ya siku 21 nitawapatia majibu ya lini maeneo yanatarajiwa kufikiwa. Aidha, nashauri maeneo husika kuunda kamati ambazo zinashirikiana nami katika ufuatiliaji.

Nawasilisha

Dkt Faustine Ndugulile (MB)

Mbunge Kigamboni

No comments:

Post a Comment